RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

JINSI YA KUKAA KATIKA UPENDO WA KWELI - ELIZABETH NGAIZA

Elizabeth Ngaiza ambaye ni mwimbaji wa nyimbo za Injili maarufu nchini Tanzania siku ya leo ameweza kutuaanadalia somo la UPENDO. Katika somo la leo kuna baadhi ya maswali ambayo aliyaandaa na amejaribu kuyajibu ili wewe na na mimi tuweze kuinua na kuiimarisha imani zetu.Sasa waweza kuungana naye kwa kusoma hiki alichokiandika.
 Elizabeth Ngaiza akiwa kwenye gari lake la kusambazia DVD zake.

WAZIA kwamba unatembea barabarani siku yenye dhoruba kali. Mawingu yanazidi kutanda. Radi inapiga na ngurumo zinasikika, kisha mvua kubwa inanyesha. Unakimbia huku na huku ukitafuta mahali pa kujikinga. Halafu, ng’ambo ya barabara unaona mahali pa kujikinga. Ni mahali imara, pakavu, na penye kuvutia. Unafurahi kama nini kupaona mahali hapo!
ElizabethNgaiza akiwa na watoto aliowatembelea ili kuwafariji na kuwapa Neno la Mungu.

Tunaishi katika nyakati zenye msukosuko. Hali za ulimwengu zinaendelea kuzorota. Hata hivyo, kuna mahali salama, kimbilio linaloweza kutukinga. Ni wapi tunapoweza kupata kimbilio hilo? Biblia inafundisha hivi: “Nitamwambia Yehova: ‘Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye nitamtegemea.’”—Zaburi 91:2.

Tunawezaje kumfanya Yehova kuwa kimbilio letu?

Hebu wazia! Yehova, Muumba anayeutawala ulimwengu mzima, anaweza kuwa kimbilio letu. Anaweza kutulinda kwa kuwa yeye ana nguvu nyingi kuliko yeyote au chochote kinachoweza kutuumiza. Hata tukiumizwa, Yehova anaweza kuondoa madhara yote mabaya. Tunawezaje kumfanya Yehova kuwa kimbilio letu? Tunahitaji kumtumaini. Isitoshe, Neno la Mungu linatusihi: “Jitunzeni katika upendo wa Mungu.” (Yuda 21) Ndiyo, tunahitaji kukaa katika upendo wa Mungu kwa kudumisha kifungo cha upendo pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Ndipo tunapoweza kuwa na hakika kwamba yeye ni kimbilio letu. Tunawezaje kudumisha kifungo hicho?

Elizabeth Ngaiza

 Taja baadhi ya njia ambazo Yehova ameonyesha upendo kwetu.
Ili tuendelee kukaa katika upendo wa Mungu, tunapaswa kutambua jinsi Yehova ametuonyesha upendo wake. Fikiria baadhi ya mafundisho ya Biblia ambayo umejifunza katika kitabu hiki. Akiwa Muumba, Yehova ametupatia dunia iwe makao yetu yenye kupendeza. Ameijaza chakula na maji mengi, mali za asili, wanyama wenye kuvutia, na mandhari maridadi. Akiwa Mtungaji wa Biblia, Mungu ametujulisha jina lake na sifa zake. Isitoshe, Neno lake husema kwamba alimtuma Mwana wake mpendwa duniani na kuruhusu ateseke na kufa kwa ajili yetu. (Yohana 3:16) Zawadi hiyo ina maana gani kwetu? Inatupa tumaini la kuwa na maisha mazuri wakati ujao.


Pia tumaini letu la wakati ujao linategemea jambo fulani ambalo Mungu amefanya. Yehova amesimamisha serikali ya kimbingu, Ufalme wa Kimasihi. Karibuni itakomesha mateso yote na kuifanya dunia iwe paradiso.
Hebu wazia! Tunaweza kuishi humo tukiwa na amani na furaha milele. (Zaburi 37:29) Kwa sasa, Mungu ametupa mwongozo wa kuishi maisha bora zaidi sasa. Pia ametupa zawadi ya sala, inayotusaidia kuwasiliana naye wakati wowote. Hizo ni baadhi ya njia chache tu ambazo Yehova ameonyesha upendo kwa wanadamu wote kwa ujumla na kwako wewe binafsi.

Unawezaje kuonyesha kwamba unathamini upendo ambao Yehova amekuonyesha?
 Hebu fikiria swali hili: Nitaonyeshaje kwamba ninathamini upendo wa Yehova? Huenda wengi wakajibu, “Kwa kumpenda pia.” Je, hivyo ndivyo unavyohisi? Yesu alisema kwamba hii ndiyo amri kuu zaidi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Bila shaka una sababu nyingi za kumpenda Yehova Mungu. Lakini je, kuhisi tu kwamba una upendo huo kunatosha kuonyesha kwamba unampenda Yehova kwa moyo, nafsi, na akili yako yote?

Je, kumpenda Mungu ni kuwa na hisia tu?
Kama Biblia inavyoonyesha, kumpenda Mungu si hisia tu. Ingawa ni muhimu kuhisi kwamba unampenda Yehova, huo ni mwanzo tu wa kumpenda kikweli. Mti wa matunda hutokana na mbegu. Ikiwa unataka kula tunda, je, utatosheka tu mtu akikupa mbegu ya tunda hilo? Hapana! Vivyo hivyo, kuhisi kwamba unampenda Yehova Mungu ni mwanzo tu. Biblia inafundisha: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Ili tumpende Mungu kikweli, lazima tuzae matunda mazuri. Ni lazima tuonyeshe kwa matendo kwamba tunampenda.—Mathayo 7:16-20.

Tunawezaje kuonyesha upendo na shukrani kwa Mungu?
 Tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu tunaposhika amri zake na kufuata kanuni zake. Si vigumu kufanya hivyo. Sheria za Yehova si nzito bali zimekusudiwa kutusaidia kuishi maisha mazuri, yenye furaha, na yenye kuridhisha. (Isaya 48:17, 18) Tunapoishi kupatana na mwongozo wa Yehova, tunamwonyesha Baba yetu wa mbinguni kwamba tunathamini kikweli yale yote ambayo ametufanyia. Inasikitisha kwamba ni watu wachache ulimwenguni leo wenye uthamini kama huo. Hatutaki kukosa uthamini kama watu fulani walioishi wakati Yesu alipokuwa duniani. Yesu aliwaponya watu kumi wenye ukoma, lakini ni mmoja tu aliyerudi kumshukuru. (Luka 17:12-17) Bila shaka tungependa kuwa wenye shukrani kama yule mtu mmoja wala si kama wale wengine tisa wasio na shukrani!

\

Comments