RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

RAIS JK KIKWETE AWAHIMIZA WAUMINI KUWACHAGUA VIONGOZI AMBAO SIO WAOVU

Rais Jakaya Kikwete amewataka viongozi wa dini nchini kuwahimiza waumini wao kuwachagua wanasiasa wasiokuwa waovu, wasiofanana na uovu au hata kuukaribia.



Amewataka kuepuka makundi ya kisiasa na wasiwape mwanya wanasiasa wenye dhamira ovu katika kutafuta madaraka kwa thamani yoyote na wawakemee wale wanaotaka kupata madaraka kwa gharama yoyote.

Alisema hayo jana wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 125 tangu kuingia kwa injili katika ukanda wa Pwani ya Tanga na Milima ya Usambara uliofanyika katika Viwanja vya Mbuyukenda jijini hapa.

“Wanasiasa wanaotaka madaraka kwa njia yoyote ile, muwanyanyapae, wakatalieni kwa macho makavu, hawa si watu wema watatufikisha pabaya,” alisema Rais Kikwete.

Alisema hayo baada ya Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini Mashariki, Dk Stephen Munga kumweleza kwamba akiwa mkuu wa nchi anao wajibu wa kuhakikisha Taifa linavuka kwa amani na usalama katika kipindi hiki kigumu cha uchaguzi.

Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, alisema katika kipindi hiki, viongozi wa madhehebu ya dini wasijiingize katika makundi ya wanasiasa kwa sababu mambo yakiharibika itakuwa hakuna pa kukimbilia.

Aliwataka viongozi wa dini watumie nyumba za ibada kuliombea Taifa livuke salama katika kipindi hiki kigumu badala ya kuwapangia vyama au viongozi wa kuwachagua.

“Tunawategemea kuwahimiza na kuwakumbusha kutumia haki na wajibu wao vizuri, muwahimize na kuwakumbusha kuwa watatakiwa kufanya mambo matatu muhimu; Kwanza, kujiandikisha, pili, kujitokeza kwenda kupiga kura na tatu kuchagua viongozi wazuri, wasiokuwa waovu, wasiofanana na uovu na kuukaribia uovu, watakaosukuma mbele gurudumu la maendeleo na kujali masilahi mapana ya jamii husika na nchi yetu.”

“Viongozi wa dini muwe kama mimi, nina wagombea wa urais 42, kama nitaonyesha kuwa upande wa mgombea yeyote kati yao, basi nitakuwa nimeharibu mchakato mzima wa uchaguzi.

“Tusiwape mwanya wanasiasa wenye dhamira ovu kuwafarakanisha Watanzania. Tuendelee kukemea matumizi mabaya ya fedha, rushwa, hila, ghiliba na hujuma katika uchaguzi. Tunapaswa kufanya hivyo tena zaidi sasa, wakati wa michakato ya ndani ya vyama vya siasa na baadaye wakati wa uchaguzi,” alisema.

Alisema hiki ni kipindi nyeti na kwamba, viongozi wa dini pamoja na Watanzania kwa ujumla wanapaswa kufahamu kuwa Tanzania haina kinga ya milele ya amani na utulivu, kama itavurugwa haitakuwa lulu ya Afrika tena kama ilivyo sifa yake.

“Tuwakemee wanasiasa wapenda madaraka kwa gharama yoyote, ambao watataka kutumia fedha kununua ushindi au ubaguzi wa rangi, kabila, dini na kadhalika, kuwabagua wapinzani wao na kujijenga kisiasa.

Nawaomba msiwasikilize wala kuwaendekeza kwani mchezo wao ni mauti yetu. Wakatalieni kwa macho makavu na kwa kweli muwanyanyapae,” alisema.

Rais Kikwete ambaye wiki hii atakuwa na kibarua cha kuongoza vikao vya kuwachuja wagombea kupitia CCM, alisema hawapaswi kukaa kimya dhidi ya watu wanaokiuka maadili na kuchochea mifarakano katika Taifa.

“Hawa si watu wema, watatufikisha pabaya. Hawaitakii mema nchi yetu. Kamwe tusiruhusu wachezee dini zetu ambazo ni mhimili muhimu sana wa amani yetu,” alisema.

Alisema tofauti na ukabila ambao pamoja na ubaya wake, unaweza kuhusisha eneo dogo, dini zinahusisha nchi nzima.

“Hakuna mtu, dini wala eneo litakalonusurika. Tutapoteza ile sifa yetu ya kihistoria ya kuwa lulu na mfano wa amani katika Afrika. Tusikubali kumchukiza Mungu akatukasirikia na kutuadhibu kwa jambo ambalo liko ndani ya uwezo wetu kulizuia lisitokee.

Kwa kweli mambo yakiharibika, hatuwezi kumlaumu mtu mwingine yeyote, bali sisi wenyewe. Katu hatuwezi kusema ni mapenzi ya Mungu, bali itakuwa ni makosa yetu wenyewe.”

Aliwaomba viongozi wa dini: “Limeni mraba wenu vizuri nasi tulime wetu. Msiwape nafasi viongozi wa siasa na hata wa dini kutumia majukwaa ya dini kuendeleza masilahi yao ya kisiasa na hasa kupandikiza chuki katika jamii.

Msiwe sehemu ya makundi ya wagombea au vyama vya siasa. Mnatakiwa msiwe na upande, muwe juu ya pande zote. Hapo ndipo mtakapofanya vizuri kazi yenu ya ulezi na kuponya Taifa iwapo kutatokea matatizo.”

Kauli ya askofu
Askofu Munga mbali na kueleza historia ya kuingia kwa injili katika eneo la Pwani ya Tanga na Milima ya Usambara, alisema kanisa hilo litaliombea Taifa livuke salama katika Uchaguzi Mkuu...

“Tunakuahidi kukuombea wewe na nchi ivuke kwa amani na salama. Wewe kama mkuu wa nchi una mzigo mzito wa kuhakikisha unatuvusha vyema.”

Alisema kilele cha maadhimisho ya miaka 125 ya kuingia kwa Injili kitakuwa Julai 12, mwaka huu katika Kanisa la Makao Makuu ya Dayosisi mjini Lushoto na zaidi ya vijana 125 watatembea kuanzia Tanga hadi Lushoto kwa kupita njia ambazo Wamisionari walipitia kwa miguu wakati wakieneza injili.

Alisema katika kipindi cha miaka 125, KKKT Dayosisi ya Kaskazini Mashariki imeendesha huduma nyingi za kuisaidia jamii ikiwa ni wajibu wake wa kutobagua kwa itikadi za kidini wala rangi.

Comments